MAISHA CHUO KIKUU

Kuna jambo laniwasha,na kunikera mtima
Ninataka kuwapasha,na munifahamu vyema
Sio jambo la kuzusha,Ni la hakika nasema
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

Wazazi ‘mejitahidi,kukulea kwa nidhamu
Nawe ukawaahidi,kuwa utajiheshimu
Ukaongeza zaidi,hutopoteza fahamu
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

‘mekuja toka nyumbani,hujui ‘boifurendi’
Leo ‘metokea nini,wavutwa na peremendi
Hata haya hauoni,na darasani huendi
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

Nyumbani ulipoketi,vyema ulijisitiri
Leo viminisiketi,watembea kwa fahari
Wavaa nguo za neti, mwili wako wadhihiri
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

Hijabu umeiasa, huivai asilani
Unafuata usasa,penseli na vimini
Na haya umeikosa,wajipamba Kama jini
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

Ulikuwa huyataki,mambo ya kujipodoa
Leo vilipustiki,tundu nyingi watoboa
Masikio hutosheki,mwatoboa mpaka pua
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

Kuswali ‘ mekuwa shida,qibla umekisahau
Unasema huna muda,unaleta na dharau
Moto ni mkali dada,tuzindukeni wadau
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

Kwa mipaka tangamana,na wote ajinabii
Jambo la kuhagiana,hilo kwao usitii
Na mikono kupeana,mola wetu haridhii
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

‘siwe chombo mwili wako,kila mtu atumie
Ipandishe hadhi yako,nafasi ‘siwapatie
Wakitaka Shari kwako,hao watu wakimbie
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

Hebu usiwe rahisi,ukajishusha thamani
Wala ‘siwape nafasi,ukabaki majutoni
Hao wanoitwa fisi,ni hatari si utani
Chuo kikuu pasiwe,pa kujifunza muozo

Mwishoni nimefikia,kwaherini waungwana
Mola ‘kitupa afia,tutazidi kujuzana
Jina mnaulizia? Naona mnanongona
Farwa Shariff nawambia,in shaa Allah tutaonana

10 thoughts on “MAISHA CHUO KIKUU

  1. Very true……awesome in shaa Allah

    Like

    1. In shaa Allah hatufanyi kuwa ni sehemu ya uozo

      Like

  2. Maa Sha Allah, Good work Farwa👏👏

    Like

  3. Farwa congrats.. good one. Keep it up.

    Like

  4. Most of Pple have changed to bad ever since they went for further studies. They have no self respect either dignity left. You are doing a great job to make them recognize themselves.

    Liked by 1 person

  5. Mashaallah Allah awajalie muwe waladun swaliha

    Liked by 1 person

    1. Shukran
      Amin 😍

      Like

  6. NAPENDA KUSHEREHESHA *** MANENO ULOTAMKA.
    NA YANGU NAYAPITISHA *** KWA YALIYO TUZUNGUKA.
    TWAONA TWAJIBORESHA **** NA KUMBE TWADHALIKIKA.

    WAZAZI NAWAULUMU *** NI SICHI KUPIGWA VITA.
    TUMEIFANYA MUHIMU *** DUNIA KUWA NI NYOTA.
    DINI TWAIONA SUMU *** LEO WANA WAZOROTA.

    MANENO YA FARWATA *** KWA MAMBO YALO CHUONI.
    KINYWA WAZI MENIWATA *** NIKIWAZA NI KWA NINI.
    NI KIPI KILOWAKUTA *** WANA WA LEO JAMANI.

    NIKUWA HAWAKUFUNZWA *** YA DINI TANGU ZAMANI.
    NDO MANA HAWAKUTUWA *** TILI KAMA FIRAUNI.
    TUWAOMBEENI DUWA *** MOLA WAMRUDIENI.

    Liked by 1 person

    1. Maa shaa Allah
      Shukran sana

      Liked by 1 person

Leave a comment